SASATEL YALIMWAGIA VIFAA VYA MAWASILIANO JESHI LA POLISI KANDA MAALUM!!

Murugenzi Mtendaji wa kampuni ya simu za mkononi Sasatel Christian Haeger akikabidhi vifaa mbalimbali vya mawasiliano kwa Kamanda wa kanda maalum ya Dar es Salaam SACP Suleiman Kova katika makabidhiano yaliyofanyika polisi kati jijini Dar es salaam leo.

Kampuni mpya ya mawasiliano ya Dovetel inayofanya biashara zake kwa jina la “Sasatel “ imetoa msaada wa simu kwa jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es salaam leo katika kusaidia jeshi hilo kupambana na uhalifu jijini.
Sasatel imetoa simu zipatazo 60 Kwa ajili ya jeshi la polisi kanda maalumu ya Dar es salaam. Madhumuni ya kutolewa kwa simu hizo ni kuunga mkono jitahada za jeshi hilo katika mapambano dhidi ya uhalifu.
Simu hizo zitatumika katika kufanya mawasiliano kati ya askari watakaokuwa doria na wananchi ambao ni raia wema watakaokuwa wanatoa taarifa kuhusu vitendo mbalimbali vya uhalifu au pale raia hao watakapokuwa na wasiwasi na mtu yoyote atakayetiliwa mashaka kwa mwenendo wake.
Vilevile askari hao wa doria wataweza kuwasiliana kwa haraka na viongozi wao watakaokuwa wanawapatia maagizo ya mara kwa mara.
Askari watakaoanza kunufaika na msaada huo ni wale askari wa doria za pikipiki, kikosi cha 999 na kadhalika.
Licha ya msaada huo Sasatel imethibitisha kwamba Gharama za muda wa maongezi zitakuwa za chini sana katika namna ambayo askari hao wataweza kuongea kwa muda mrefu kulingana na mazingira ya kazi zao.
Katika kuleta ufanisi kuhusu mawasiliano askari wa doria na wananchi kila eneo katika kanda maalum watapewa namba hizo na kuorodheshwa katika vituo vya Polisi vyote vya kanda maalaum ya Dar es Salaam ili kurahisisha utendajiwa wa askari wa Doria.
Kutokana na msaada huo kamanda wa polisi Dar e salaam Kanda Maalum SACP Suleiman Kova, ameishukuru kampuni ya Sasatel kwa kutambua kwa haraka na umuhimu na kuthamini kazi za jeshi la polisi kwa hatua ambayo kampuni hiyo imeonyesha, Licha ya shughuli za kibiashara Kampuni hiyo imeonyesha kujali maslahi ya wananchi ikiwa na pamoja na usalama wao

You liked this post? Subscribe via RSS feed and get daily updates.

0 comments:

Post a Comment